Saturday 25 April 2015

ROSTI YA VIAZI MBATATA NA SAMAKI


Karibu tena katika jikoni kulikoni. Jikoni leo tutapika rosti la viazi mbatata na samaki wa kukaanga . mlo huu watu wengi uupika lakini leo tutapika tofauti kidogo na tupikavyo majumbani  kwetu ili kupata ujuzi mwingine wa kupika chakula hiki na kupata radha tofauti na tamu kuliko unayopata siku zote.

Mahitaji ya rosti ya viazi mbatata

  • Viazi  mbatata ¼
  • Nyanya maji 3
  • Kitunguu maji 1
  • Kitunguuu swaumu kijiko 1
  • Binzari ya pilau ½ kijiko
  • Mdalasini ½ kijiko
  • Nyanya ya kopo 1
  • Pilipili mboga/kuwasha
  • Karoti na hoho 1
  • Chumvi kiasi
  • Limau 1
  • Mafuta ½ chupa

Jnsi ya kuandaa rosti la viazi mbatata

  1. Menya viazi na katakata vipande vidogo vidogo na kuvisafisha vizuri kwenye chombo safi, kisha anza kusafisha nyanya  karoti, vitunguu na karoti. Andaaa vitunguu swaumu kwa kuvimenya na kuviponda,kisha katakata vitunguu maji na nyanya .
  2. Chukua kiaangio Kaanga viazi vikiiva weka pembeni, katika sufuria kaanga vitunguu maji hadi viwe vya kawahia weka pilpili mboga/kuwasha na karoti.
  3. Kaanga vikikaribia kuiva weka nyanya maji kaanga vizuri hadi ziive, weka nyanya ya kopo na limau kiasi ila usisahau kuweka chumvi.
  4. Ikisha iva, changanya na viazi ulivyovikaanga na rosti, uku ukiendelea kuvichanganya taratibu, hakikisha viazi avirojeki sana.

Mahitaji ya samaki

  • Samaki 1
  • Pilipili manga/mtama ½ kijiko
  • Tangawizi ½ kijiko
  • Kitunguu swaumu
  • Chumvi kiasi

Jinsi ya kuandaa samaki

  1. Safisha samaki kwa maji safi, kuondoa magamba na vitu vya tumboni na mapezi
  2. Muweke viungo kwa kupaka sehemu zote kwa kumpaka pilipili, tangawizi, kitunguu swaumu pamoja na chumvi, subiri kwa muda wa dakika 30 viungo vikolee kwenye samaki wako.
  3. Weka kikaangio mafuta, mafuta yakisha pata moto, kaanga samaki uku baada ya muda unamgeuza upande wa pili.
  4. Samaki akiiva weka kwenye chombo chako kisafi kisha mimina rosti lako la viazi mbatata juu ya samaki na hapo mboga yako itakuwa tayari kwa kuliwa unaweza kula rosti lako kwa wali ama ugali.
    rosti ya  viazi mbatata na samaki


Thursday 23 April 2015

MCHANYATO WA NDIZI,NYAMA NA MAHARAGE


Mchanyato wa ndizi, nyama na maharage ni chakula kikuu cha kabila la wahaya na wachaga. chakula hiki wanakiita mchanyato kwa sababu wa mchanganyiko wa vyakula mbali mbali.

Chakula hiki upikwa kwa kutumia ndizi bukoba ama ndizi mshale. Jikoni leo tutapika mchanyato wa ndizi bukoba,nyama na maharage.

Mahitaji
  • Nyama  ¼  kilo
  • Ndizi mbichi kubwa 12
  • Maharage vikombe 2
  • Chumvi kijiko cha chakula 2
  • Nyanya kubwa  4 zilizoiva vizuri
  • Vitunguuu vikubwa 2
  • Maji kiasi cha vikombe 4

Njia
  1. Loweka maharage kwa muda wa saa tatu
  2. Osha na katakata nyama na kuibandika nyama jikoni tayari kwa kuichemsha.
  3. Pika maharage mpaka yakaribie kuiva.
  4. zikisha iva vyote changanya nyama katika maharage na endelea kupika.
  5. Menya ndizi na kuzikatakata katikati au nusu ukipenda .
  6. Changanya ndizi katika  katika nyama na maharage    
  7. Katakata vitunguu na nyanya na kuviongeza kwenye mchanyato
  8. Kisha weka chumvi na mafuta ili chakula chako kiwe na radha tamu ila usisahau kuweka maji katika chakula chako ili kuivisha chakula na kukupa mchuzi au lojo ya kutosha.
  9. Funika na pika polepole mpaka ndizi ziwe laini.
  10. Pakua na kula chakula hicho kingali moto.

mhanyato wa ndizi bukoba,nyama na maharage

Monday 20 April 2015

MCHANGANYIKO WA MAHARAGE MAKAVU NA NYAMA


Kama ilivyo ada kila siku tunahitaji kufahamu kilichpo jiikoni. Jikoni leo tumeandaa mchanganyiko wa maharage na nyama. Nyama na maharage  ni aina ya protini ambayo hujenga mwili wa binadamu, vilevile nyama hutupatia vitamini B, chuma, fosiforasi na mafuta.
Maharage pia ni aina ya chakula jamii ya wanga,Ili kuweza kuhakikisha kwamba mwili umepata kiasi cha kutosheleza cha protini kwa siku ni vizuri kuchanganya maharage na nyama.
Jambo hili lina maana sana kwa sababu protini iliyoko katika maharage sio kamili inaweza kukamilishwa kwa kuchanganywan na vyakula vingine vyenye asili ya nyama. Ili mchanganyiko wako uwe mtamu, unatakiwa kupikwa vizuri na mapishi yabadilike siku hadi siku.

Mahitaji
  • Maharage makavu kikombe cha chai 1
  • Nyama bila mfupa ¼ kilo
  • Vitunguu maji
  • Nyanya kubwa za kuiva 3
  • Binzari au viungo vya mchuzi kijiko 1
  • Mafuta kijiko cha chakula 2
  • Pilipili ukipenda
  • Hoho na karoti
  • Limau 1
Njia

  1. Chagua maharage, safisha na kuyaloweka kwa muda wa masaa matatu
  2. Baada ya kuloweka maharage yako. Pika maharage kwa maji yale yale uliyolowekea mpaka yalainike.
  3. Osha nyama ikatekate vipande vidogo vidogo, weka maji ya limau au ndimu.
  4. Katakata vitunguu, hoho, karoti na nyanya. Kaanga vitunguu, hoho na karoti kisha weka nyama na kaanga. Ongeza  nyanya, chumvi,pilipili, na viungo vya mchuzi, endelea kupika mpaka nyama iive
  5. Nyama ikisha iva weka maharage yaliyoiva bila maji, koroga na kupika kwa muda mfupi.
  6. Ongeza maji ya kutosha ili kufanya mchuzi uwe mzito. Acha ichemke kwa muda mfupi.
  7. Tayari mboga yako itakuwa immeiva pakuwa na waweza kula mboga hiyo kwa ugali au wali  ili mlo wako ukamilike ni lazima uwe na mboga mboga za majani pembeni au matunda
wali na mchanganyiko wa maharage na nyama

Saturday 18 April 2015

MCHANGANYIKO WA MBOGAMBOGA NA BIRIANI

Naam, kama ilivyo ada kila siku watu wanapenda kujaa kilichopo jikoni. jikoni leo tunaandaa mchanganyiko wa mboga mboga na biriani. leo nimependa kuwaandalia vyakula hivi kwasababu vinapendwa na watu wengi, pia unashauriwa kuandaa chakula ambavyo vinakidhi mahitaji yote yanayohitajika mwili ndiomana nikaamua kuandaa mchanganyiko wa mboga mboga kwa biriani.

Mahitaji ya biriani
  • Nyama ½ kilo
  • Mchele ½ kilo
  • Kitunguu swaumu na vitunguu maji
  • Maziwa ya mgando ½ kikombe
  • Giligilani
  • Nyanya ya kopo  1
  • Zabibu kavu kijiko cha chakula 3
  • Dengu zilizoondolewa maganda kikombe 1
  • Mdalasini ¼ kikombe
  • Iriki
  • Maji kiasi cha vikombe 8
  • Rangi ya chakula (ukipenda)
  • Pilipili manga (ukipenda)
  • Karoti na hoho
  • Mafuta vikombe 2 au zaidi
  • Chumvi

Mahitaji ya mbogamboga mchanganyiko
  • Karoti
  • Nyanya zilizoivya vizuri
  • Kabichi
  • Pilipili hoho
  • Matango
  • Vitunguu
  • Chumvi
  • limau/ ndimu
  • Mafuta ya kula
Njia
  1. Chagua, safisha na chemsha dengu.
  2. Chagua mchele na pepeta kuondoa chenga
  3. Osha, katakata nyama weka katika chombo chako cha kupikia
  4. Ponda mdalasini mpaka uwe laini na uchekecha. Ponda vitunguu saumu, pamoja na giligilani na iriki kila moja tofauti tofauti.
  5. Weka maziwa ya mgando katika nyama, ongeza na dengu zilizochemshwa na kuiva kiasi, viungo vilivyo pondwa kama kitunguu swaumu, giligilani na iriki, nyanya ya kopo na unga wa mdalasini pamoja na viungo vingine kama hoho na karoti kidogo.
  6. Chemsha mafuta, kaanga vitunguu maji mpaka viwe kahawia. Chuja vitunguu na mimina mafuta ya moto katika nyama uliyotayarisha pamoja na viungo. Tia nusu ya vitunguu vilivyokaangwa,katika nyama na ubandike jikoni. Chemsha polepole katika mafuta, angalia nyama isishike chini. Endelea kuchemsha mpaka nyama inalainika uku ukiangalia isikauke.
  7. Chemsha maji pamoja na chumvi. Osha mchele na tia ndani ya maji yaliyochemshwa na chumvi.ongeza rangi ya chakula ukipenda. Mchele ukiiva ipua na uchuje kutoa maji yote.
  8. Rudisha wali kiasi katika chombo unachopikia birani yako, weka nyama na mchuzi juu yake nyunyuzia vitunguu vilivyobaki. Funika na wali mwingine kiasi. Endelea kufanya hivyo mpaka nyama, wali na vitunguu viishe. Maliza kwa kufunika wali juu.
  9. Weka chungu juuu ya moto, na palia makaa ya moto juu kiasi, vikiivya ondoa weka katika chombo safi. Kisha andaa mchanganyiko wako wa mboga mboga.
  10. Chambua kabichi na kusafisha jani moja moja  vizuri katika maji ya chumvi ili kuondoa uchafu na mchanga unaokaa katika kabichi.
  11. Safisha mboga nyingine zote katika maji ya chumvi.
  12. Paruza karoti kwa kuondoa uchafu, katakata vipande vyembamba au kuna kwenye kikunio (greta)
  13. Katakata kabichi vipande vyembamba sana na katakata matango mduara au umbo lolote la jingine.
  14. Katakata vitunguu na nyanya,viwe vidogo vidogo au umbo lolote zuri.
  15. Kamua limau na chuja maji.
  16. Changanya kabichi, karoti nyanya,vitunguu kwenye bakuli, koroga vizuri. Ongeza chumvi.
  17. Ongeza mafuta na maji ya limau/ siki na uchanganye vizuri
  18. Panga tango juu ya pilipili hoho zilzo katika maumbo mazuri.

Biriani
Mchanganyiko ni tayari. Mchanganyiko huu hatuupiki jikoni kwa sababu ya kuwacha mchanganiko wetu wa mbogamboga kubaki na ukijani na unashauriwa kiafya kutochemsha mboga za majani kwa sababu unapochemsha mbogamboga unaondoa virutubisho vilivyopo kwenye mboga mboga au kama unachemsha chemsha kidogo tuu. Mchanganyiko huo wa mboga mboga waweza kuuandaliwa na biriani yako uliyopika na tayari kwa kuliwa, pia unaweza kula mchanganyiko huo wa mboga mboga katika pilau au vyakula vingine vikavu.

Friday 17 April 2015

kisamvu cha nazi



Naaam leo katika jikon leo tutaandaa kisamvu cha nazi, kwanza kabisa napenda kukueleza ya kuwa mboga za majani zinahitajika mwilini kwa sababu zina aina nyingi za  madini  na vitamini, hasa vitamini A na C vitu ambavyo ni vya lazima katika kukuza na kulinda mwili usipatwe na maradhi.

 Pia husaidia chakula kuyeyushwa haraka tumboni. Jikon leo tutaandaa kisamvu cha nazi na unashauriwa kupika mboga za majani mara baada ya kuzichuma. 

 Mahitaji
kisamvu

chumvi





nazi
kitunguu
kitunguu swaumu



 Njia
1.      Chambua kisamvu, kisafishe vizuri kwa maji na chumvi ilikuondoa uchafu na wadudu, na ukitwange kwenye kinu ukichanganya na vitunguu swaumu mpaka kiwe laini, kuna nazi na uchuje tui zito (tui bubu) na jepesi.

2.      Anza kuchemsha kisamvu,uku ukiendelea kutayarisha viungo. Katakata kitunguu maji, hoho na karoti, kisamvu kikishaanza kuiva na maji kukauka, weka kitunguu,hoho, karoti na chumvi.kisha weka tui jepesi ili kiendelee kuiva na kuwa laini zaidi 
3.      Tui likikauka weka tui zito pika hadi tui likauke kabisa hapo ndo utaona utamu wa kisamvu.
4.      Kisamvu hiki kinaweza kuliwa na wali au ugali, kisamvu ni mboga inayotupatia virutubiho na madini mwilini lakini kisamvu hicho hicho  kikiwa shambani mti wake ni kuni, mizizi yake unaweza ukapata unga wa ugali, muhogo unaweza kupika  ikawa kitafunwa ama kifungua kinywa kwa kushushia na chai, maji vilevile unaweza kupika uji wa mhogo.



5.     Jiandae  na kwa mapishi ya mbogamboga mchanganyiko. Usichoke endelea kusoma blog hii ili kujua mambo mengi zaidi kuhusiana na vyakula.