Saturday 18 April 2015

MCHANGANYIKO WA MBOGAMBOGA NA BIRIANI

Naam, kama ilivyo ada kila siku watu wanapenda kujaa kilichopo jikoni. jikoni leo tunaandaa mchanganyiko wa mboga mboga na biriani. leo nimependa kuwaandalia vyakula hivi kwasababu vinapendwa na watu wengi, pia unashauriwa kuandaa chakula ambavyo vinakidhi mahitaji yote yanayohitajika mwili ndiomana nikaamua kuandaa mchanganyiko wa mboga mboga kwa biriani.

Mahitaji ya biriani
  • Nyama ½ kilo
  • Mchele ½ kilo
  • Kitunguu swaumu na vitunguu maji
  • Maziwa ya mgando ½ kikombe
  • Giligilani
  • Nyanya ya kopo  1
  • Zabibu kavu kijiko cha chakula 3
  • Dengu zilizoondolewa maganda kikombe 1
  • Mdalasini ¼ kikombe
  • Iriki
  • Maji kiasi cha vikombe 8
  • Rangi ya chakula (ukipenda)
  • Pilipili manga (ukipenda)
  • Karoti na hoho
  • Mafuta vikombe 2 au zaidi
  • Chumvi

Mahitaji ya mbogamboga mchanganyiko
  • Karoti
  • Nyanya zilizoivya vizuri
  • Kabichi
  • Pilipili hoho
  • Matango
  • Vitunguu
  • Chumvi
  • limau/ ndimu
  • Mafuta ya kula
Njia
  1. Chagua, safisha na chemsha dengu.
  2. Chagua mchele na pepeta kuondoa chenga
  3. Osha, katakata nyama weka katika chombo chako cha kupikia
  4. Ponda mdalasini mpaka uwe laini na uchekecha. Ponda vitunguu saumu, pamoja na giligilani na iriki kila moja tofauti tofauti.
  5. Weka maziwa ya mgando katika nyama, ongeza na dengu zilizochemshwa na kuiva kiasi, viungo vilivyo pondwa kama kitunguu swaumu, giligilani na iriki, nyanya ya kopo na unga wa mdalasini pamoja na viungo vingine kama hoho na karoti kidogo.
  6. Chemsha mafuta, kaanga vitunguu maji mpaka viwe kahawia. Chuja vitunguu na mimina mafuta ya moto katika nyama uliyotayarisha pamoja na viungo. Tia nusu ya vitunguu vilivyokaangwa,katika nyama na ubandike jikoni. Chemsha polepole katika mafuta, angalia nyama isishike chini. Endelea kuchemsha mpaka nyama inalainika uku ukiangalia isikauke.
  7. Chemsha maji pamoja na chumvi. Osha mchele na tia ndani ya maji yaliyochemshwa na chumvi.ongeza rangi ya chakula ukipenda. Mchele ukiiva ipua na uchuje kutoa maji yote.
  8. Rudisha wali kiasi katika chombo unachopikia birani yako, weka nyama na mchuzi juu yake nyunyuzia vitunguu vilivyobaki. Funika na wali mwingine kiasi. Endelea kufanya hivyo mpaka nyama, wali na vitunguu viishe. Maliza kwa kufunika wali juu.
  9. Weka chungu juuu ya moto, na palia makaa ya moto juu kiasi, vikiivya ondoa weka katika chombo safi. Kisha andaa mchanganyiko wako wa mboga mboga.
  10. Chambua kabichi na kusafisha jani moja moja  vizuri katika maji ya chumvi ili kuondoa uchafu na mchanga unaokaa katika kabichi.
  11. Safisha mboga nyingine zote katika maji ya chumvi.
  12. Paruza karoti kwa kuondoa uchafu, katakata vipande vyembamba au kuna kwenye kikunio (greta)
  13. Katakata kabichi vipande vyembamba sana na katakata matango mduara au umbo lolote la jingine.
  14. Katakata vitunguu na nyanya,viwe vidogo vidogo au umbo lolote zuri.
  15. Kamua limau na chuja maji.
  16. Changanya kabichi, karoti nyanya,vitunguu kwenye bakuli, koroga vizuri. Ongeza chumvi.
  17. Ongeza mafuta na maji ya limau/ siki na uchanganye vizuri
  18. Panga tango juu ya pilipili hoho zilzo katika maumbo mazuri.

Biriani
Mchanganyiko ni tayari. Mchanganyiko huu hatuupiki jikoni kwa sababu ya kuwacha mchanganiko wetu wa mbogamboga kubaki na ukijani na unashauriwa kiafya kutochemsha mboga za majani kwa sababu unapochemsha mbogamboga unaondoa virutubisho vilivyopo kwenye mboga mboga au kama unachemsha chemsha kidogo tuu. Mchanganyiko huo wa mboga mboga waweza kuuandaliwa na biriani yako uliyopika na tayari kwa kuliwa, pia unaweza kula mchanganyiko huo wa mboga mboga katika pilau au vyakula vingine vikavu.

No comments:

Post a Comment